WAKULIMA WANUFAIKA NA MBOLEA YA BEI NAFUU KIMININI TRANS NZOIA.


Zaidi ya wakulima 41 kutoka ushirika wa KAMISSA eneo bunge la Kiminini wamepokea mbolea ya bei nafuu kupitia kwa mradi wa serikali kuu kwa ushirikiano na new KPCU ambapo wakulima wanalipia 60% huku serikali ikilipia 40%.
Kwenye hafla ya kutoa mbolea hiyo Waziri wa Kilimo Kaunti ya Trans Nzoia Mary Nzomo amesema hatua hii ni njia moja ya kusaidia wakulima kutokana na kupanda kwa gharama ya mbolea mbali na kuboresha uzalishaji wa Kahawa Kaunti ya Trans Nzoia.
Wakati huo huo Nzomo amesikitikia kuendelea kudorora kwa kiwango cha uzalishaji wa kahawa Kaunti hiyo kwa kila mche akisema msaada huo utapiga jeki uzalishaji huo.
Msimamizi wa shirika la Kahawa la New KPCU Kaunti ya Trans Nzoia na Bungoma Moses Wandwasi amesema wakulima hao wamepokea magunia 145 ya mbolea akitoa wito kwa wakulima zaidi kujisajili ili kufaidi mbolea hiyo.