WAKAZI POKOT MAGHARIBI WATAKIWA KUJISAJILI KWA WINGI KUWA WAPIGA KURA.


Awamu ya pili ya zoezi la kuwasajili wapiga kura wapya likiingia wiki ya pili, miito imeendelea kutolewa kwa vijana ambao hawajajisajili kuhakikisha kuwa wanafika katika vituo vya kuwasajili wapiga kura ili waweze kusajiliwa.
Wa hivi punde kutoa wito huo ni mwaniaji wa kiti cha mwakilishi wadi ya Siyoi kaunti hii ya Pokot magharibi Esther Serem ambaye amesema kuwa ni kupitia kusajiliwa kuwa wapiga kura ndipo wataweza kuwa katika nafasi ya kuwachagua viongozi wanaofaa.
Aidha Serem amewataka wakazi wa kaunti hii kutokubali kushawishiwa kuwapigia kura watu ambao hawatakuwa wa manufaa kwao bali kufanya uamuzi wao wa busara ifikiapo Agosti 9.
Wakati uo huo Serem amewataka vijana katika kaunti hii kuzingatia zaidi amani hasa msimu huu wa siasa za uchaguzi mkuu ujao, na kutokubali kutumika na wanasiasa kuvuruga amani kwa misingi ya tofauti za vyama.