VIONGOZI KAUNTI YA POKOT MAGHARIBI WAMETAKIWA KUINGILIA KATI NA KUOKOA HALI YA HOSPITALI YA KAPENGURIA INAYO ANGAMIA

Hali ya Hospitali ya Rufaa ya Kapenguria inazidi kudorora huku wakazi wakiendelea kuhangaika kwa kutafuta dawa na matibabu kutoka kwenye hospitali za binafsi.
Baada ya udadisi kutoka kwa kituo hiki cha Kalya Redio, tulipata fursa ya kumhoji mmoja wa waliowaleta watlgonjwa wao kwenye hospitali hiyo, na kulingana na yeye, si dawa tu zinazokosekana kwenye hospitali hiyo bali wagonjwa wamelazimika kununua maji kwa shilingi hamsini kwa kila lita ishirini ya maji.
Ametaja pia mazingira ya hospitali hiyo kuwa changamoto kubwa hasa baada ya maji kuisha huku wauguzi wakikosa kuwawajibikia wagonjwa hao kutokana na ukosefu wa dawa na vifaa vingine vya matibabu.
Inadaiwa hali si hali kwenye zahanati nyingine kwenye Kaunti hii ya Pokot Magharibi, tatizo likiwa lilo hilo la kukosekana kwa dawa na vifaa vingine vya matibabu. Ni wiki chache tu zilizopita ambapo wakazi wa Eneo la Kacheliba walilalamikia hali sawa na hiyo.
Vilevile jamaa mmoja anadaiwa kutembea kwa miguu kutoka Eneo la Lomut hadi Kapenguria kutafuta matibabu baada ya kukosekana kwa dawa kwenye zahanati za eneo hilo, hali ambayo imesababisha jamaa huyo kufariki dunia punde tu alipofika Mji wa Kapenguria jambo ambalo wakazi wa Kaunti hii wanazidi kukemea uongozi wa Gavana John Lonyangapuo.
Huu ni wito kwa serikali ya Gavana John Lonyangapuo kuhusiana na hali mbaya ya Hospitali ya Rufaa ya Kapenguria na zahanati nyingine katika Kaunti hii.