TAHADHARI YATOLEWA KWA UMMA DHIDI YA MATAPELI WANAOJIFANYA KUWA MAAFISA WA KENYA POWER.

Visa vya utapeli kwa kutumia jina la kampuni ya umeme ya Kenya power vimeripotiwa kukithiri katika kaunti hii ya Pokot magharibi cha hivi punde kikihusu shule ya upili ya wasichana ya St Bakhita katika kaunti hii.
Kulingana na mwalimu mkuu wa shule hiyo Grace Kakuko, alipokea simu kutoka kwa watu waliojitambulisha kuwa maafisa wa Kenya power wakimwitisha kiasi Fulani cha fedha ili kuboresha huduma za umeme katika shule hiyo akijipata katika mtego huo na kuwatumia shilingi alfu saba kabla ya kubaini kuwa ametapeliwa.
Ametoa wito kwa umma kuchukua tahadhari dhidi ya utapeli huo na kuwataka kuwa makini na watu wanaowataka kulipa huduma zozote kutoka Kenya power na kuhakikisha kabla ya kutuma fedha kwa mtu yeyote.
Meneja wa kampuni hiyo kaunti hii Milimo Amusavi amethibitisha kuwepo utapeli wa aina hiyo akisema wahusika kwa majina Roselyne Ombati na Keter wamekuwa wakiwatapeli wananchi wakidai kuwa wafanyikazi wa Kenya power, akiwataka wakazi kutoshawishiwa na yeyote kutoa fedha kwa huduma za kampuni hiyo.