SHULE YA CANON PRICE TAMKAL YAFUNGWA KWA MAJUMA MAWILI

Shule ya upili ya Canon price Tamkal eneo bunge la Sigor imefungwa kwa muda wa majuma mawili.
Hii ni baada ya wanafunzi wa shule hiyo kuandamana usiku wa kuamkia jumatatu wiki hii wakilalamikia matokeo duni katika mtihani wa kitaifa kwa kidato cha nne KCSE huku wakimshutumu mwalimu mkuu wa shule hiyo kwa kuchangia matokeo hayo.
Aidha wanafunzi hao walitaka mwalimu huyo kupewa uhamisho kwa madai amehudumu katika shule hiyo kwa muda mrefu.
Hata hivyo akijitetea Erustus Masambaka alipuuzilia mbali madai hayo akisema kuwa masaibu yake yamechangiwa na hatua yake kudinda kuwasaidia wanafunzi kuiba mtihani wa kcse mwaka 2020.
Aidha Masambaka amedai kuwepo watu ambao wanampiga vita baada ya kuongoza shule hiyo kuanza kurekodi matokeo bora katika mitihani ya miaka ya awali.