SHINIKIZO ZATOLEWA KWA MAGOHA KUJIUZULU.

Na Benson Aswani
Kufuatia ongezeko la visa vya mikasa ya moto shuleni mwakilishi wadi ya Bartabwa katika kaunti ya Baringo Ruben Chepsongol sasa anamtaka waziri wa elimu Prof George Magoha kujiuzulu wadhifa wake.
Akiongea mjini Kabarnet Chepsongol ambaye pia ni kiranja wa wengi kwenye bunge la kaunti ya Baringo amesema kuwa waziri Magoha ameshindwa kutoa uongozi unaofaa kwenye wizara ya elimu.
Chepsongol amesema kuwa iwapo waziri Magoha hatajiuzulu kwa hiari basi rais Uhuru Kenyatta anastahili kuingilia kati na kumwondoa kwenye wizara hiyo na pia kuagiza kuanzishwa uchunguzi kubaini sababu ya kutokea kwa mikasa hiyo ya moto.
Aidha Chepsongol amesema utovu wa nidhamu miongoni mwa wanafunzi umechangiwa na wazazi kutelekeza majukumu yao huku pia akipendekeza kurejeshwa kwa adhabu ya kiboko shuleni.