SERIKALI YALENGA KUIMARISHA USALAMA KATIKA BONDE LA KERIO.

Na Benson Aswani
Serikali inalenga kutuma vikosi maalum vya maafisa wa usalama katika eneo la bonde la kerio katika juhudi za kuimarisha oparesheni ya kusaka wezi wa mifugo.
Mshirikishi wa utawala eneo la bonde la ufa George Natembeya amesema kuwa hatua hiyo imechochewa na kuendelea kushambuliwa kwa wenyeji na wezi hao ambapo watu watano wameuliwa ndani ya wiki mbili pekee.
Aidha Natembeya amesema kuwa mkutano utakaowajumuisha wakuu wa usalama na viongozi wa kisiasa kutoka kaunti za Pokot magharibi, Elgeyo marakwet na Baringo utafanyika hivi karibuni kujadili jinsi ya kufanikisha oparesheni ya kuwasaka wahalifu hawa.
Katika visa vya hivi punde vya uvamizi mama na wanawe wawili waliuliwa kwa kupigwa risasi na wahalifu kabla ya kumuua afisa wa kilimo eneo la Ngachar kaben huko Elgeyo marakwet huku mtu mmoja akiuliwa sirmaj chesogon mpakani pa kaunti hii ya pokot magharibi na Elgeyo marakwet.
Wakazi sasa wanatoa wito kwa serikali kuweka mikakati ya kuwahakikishia usalama.