OPARESHENI YA KUWAFURUSHA WAKAZI KATIKA MSITU WA MAKUNGA TRANS NZOIA YAANZISHWA.

Serikali imeanzisha oparesheni ya kuwahamisha wakazi ambao wameuvamia msitu wa makunga eneo bunge la Saboti kwenye kaunti ya Trans nzoia na ambako wanaendeleza shughuli za kilimo.
Akizungumza baada ya kikao na wadau mbali mbali ambao watahusika katika kufanikisha oparesheni hiyo kamishina wa kaunti hiyo Sam Ojwang amesema shughuli hiyo itaendelezwa kwa ekari 500 za msitu huo akionya kuwa yeyote atakayepatikana katika msitu huo atakabiliwa kisheria.
Amewataka wanaomiliki silaha hatari ambazo wanatumia kutatiza oparesheni hiyo kwa kuwakabili maafisa wa polisi kuzisalimisha la sivyo wakabiliwe kikamilifu.
Wakati uo huo Ojwang amewalaumu baadhi ya viongozi wa kisiasa kaunti hiyo anaodai kuwa wamewachochea wakazi kuvamia msitu huo kama njia moja ya kujipatia umaarufu wa kisiasa akisema kuwa wanafuatiliwa kwa karibu na vitengo vya ujasusi.