MCHUJO WA UDA WAAHIRISHWA KATIKA WADI NNE POKO MAGHARIBI


Shughuli ya mchujo wa chama cha UDA kaunti hii ya Pokot magharibi unapoandaliwa leo huenda zoezi hilo likakosa kuandaliwa leo katika wadi za Endough na Riwo eneo bunge la Kapenguria na wadi za tapach na Lelan eneo bunge la Pokot Kusini.
Kulingana na msimazi wa uchaguzi katika chama cha UDA kaunti hii Ann Wanjiku hali hii imetokana na uhaba wa mafuta ambao umepelekea kutowasilishwa kwa wakati vifaa vya uchaguzi maeneo ya Endough na Riwo licha ya maandalizi yote kwa ajili ya uchaguzi huo kukamilika.
Aidha Wanjiku amesema uchaguzi katika wadi za Tapach na Lelan umelazimika kuahirishwa kutokana na taarifa za kukanganya kuhusu maelewano miongoni mwa wagombea wa maeneo hayo hali ambayo ilivuruga maandalizi ya uchaguzi huo akisema kuwa zoezi hilo sasa litaandaliwa jumatatu juma lijalo katika wadi hizo nne.
Wanjiku ameomba radhi kwa wagombea nyadhifa hizo pamoja na wananchi wa maeneo hayo na kuwataka kuendelea kuwa na subira akiwahakikishia kuwa zoezi hilo litaandaliwa siku ya jumatatu juma lijalo.