GAVANA LONYANGAPUO ATETEA UTENDAKAZI WAKE POKOT MAGHARIBI.


Gavana wa kaunti hii ya Pokot magharibi John Lonyangapuo ametetea utendakazi wake tangu alipochaguliwa kuwa gavana wa kaunti hii.
Akizungumza katika hafla ya kuzindua pikipiki za sacco ya WEPESA mjini Makutano, gavana Lonyangapuo amesema kuwa sacco hiyo ni moja ya miradi ambayo ameanzisha kaunti hii ambapo wakazi wengi wamenufaika na kuimarika kiuchumi.
Aidha Lonyangapuo ametaka maafisa kutoka sacco hiyo kwa ushirikiano na maafisa katika wizara ya biashara katika kaunti hii kuhakikisha sacco hiyo inaimarika zaidi, huku akisisitiza kuwa serikali yake imejitolea kuhakikisha kuwa mfanyibiashara kaunti hii analindwa.
Kwa upande wake waziri wa ardhi na mipangilio ya miji katika kaunti hii Augustine Lotodo ametoa wito kwa wafanyibiashara mjini makutano kushirikiana na idara yake kuhakikisha kuwa wanafanyia shughuli zao katika mazingira bora.