SERIKALI KULEGEZA MASHARTI YA KUKABILI WIZI WA MIFUGO BARINGO.
Serikali ya kitaifa itaangazia upya mikakati iliyowekwa awali kukabili tatizo la usalama kwenye kaunti ya Baringo na maeneo jirani.
Akizungumza baada ya mkutano na viongozi wa eneo bunge la Tiati, mshirikishi wa utawala eneo la bonde la ufa George Natembeya amesema baadhi ya mikakati hiyo ikiwemo matumizi ya vizuizi imechangia pakubwa kuathirika shughuli za biashara na usafiri katika kaunti hiyo.
Amesema kwa sasa wakazi wataruhusiwa kutembea kwenye sehemu mbali mbali bila kuhangaishwa na maafisa wa polisi wanaolinda doria.
Polisi wamekuwa wakiendesha oparesheni katika kaunti ya Baringo na Kapedo kuanzia mwezi Aprili ili kuwakabili wezi wa mifugo ambao wanaendelea kusababisha maafa.
Ni tangazo ambalo limeshabikiwa pakubwa na baadhi ya viongozi wa eneo hilo.
Baadhi ya viongozi wa Baringo wamekuwa wakipinga vikali oparesheni hiyo wakisema kuwa raia wasiokuwa na hatia wanakandamizwa na maafisa wa polisi.